February 2, 2017

Kiini cha Wanafunzi kufeli kidato cha nne chaanikwa

KUPELEKWA wanafunzi waliopata alama za chini katika mtihani wa darasa la saba na hivyo kushindwa kumudu masomo ya sekondari, kumetajwa kuwa ni moja ya sababu za kufanya vibaya kwa shule sita za Mkoa wa Dar es Salaam katika matokeo ya Kidato cha Nne mwaka jana.

Mbali ya hilo, imebainika kuwa viashiria vya matokeo mabaya kwa shule hizo vilianza kuonekana katika matokeo ya mtihani wa majaribio, jambo ambalo liliwafanya wakurugenzi kuwaandikia barua wakuu wa shule hizo kuongeza juhudi katika masomo ili kuepuka matokeo mabaya katika mtihani wa mwisho.

Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) juzi lilitangaza matokeo ya mtihani wa kidato cha nne kwa mwaka 2016 na kubainisha ufaulu wa jumla kwa watahiniwa wa shule kuongezeka kwa asilimia 2.44, idadi ya watahiniwa waliopata alama za kuwawezesha kuendelea kidato cha tano kuwa chini kwa miaka mitatu mfululizo.

Hata hivyo, katika matokeo hayo, shule sita za mkoa wa Dar es Salaam zimekuwa miongoni mwa shule 10 za mwisho kitaifa. Shule hizo ni Kitonga, Nyeburu, Kidete, Mbopo, Mbondole na Somangila Day, ambazo katika kundi hilo zimo pamoja na Masaki (Pwani), Dahani (Kilimanjaro), Ruponda (Lindi) na Makiba (Arusha).

Wanafunzi wasio na uwezo
Gazeti hili jana na juzi lilitembelea baadhi ya shule hizo na kuzungumza na walimu, watendaji wa elimu na watendaji wa serikali wa kata pamoja na wanafunzi, na katika mazungumzo hayo, zimetajwa sababu mbalimbali zikiwamo za kuchukuliwa kwa wanafunzi wanaopata alama za chini darasa la saba, na suala la umbali kwa wanafunzi kutoka wanakoishi hadi shule walizopangiwa kusoma.

Shule zilizotembelewa ni Kitonga, Mbondole zilizopo katika Kata ya Msongola na Sekondari ya Nyeburu iliyopo katika Kata ya Chanika, zote katika Manispaa ya Ilala.

Mmoja wa walimu katika shule hizo, alisema kumekuwa na tabia ya kupeleka wanafunzi wenye ufaulu wa chini ya alama zinazotakiwa za ufaulu wa darasa la saba ambazo ni 250, hivyo kusababisha kuchukua wanafunzi wasio na uwezo darasani.

“Sababu zinaweza kuwa nyingi, lakini hili la kuchukua wanafunzi ambao walifeli darasa la saba kiasi cha kushindwa kumudu masomo ya sekondari lipo. Mwanafunzi anatakiwa kupata alama 250, lakini wapo wanafunzi ambao wamepata hata alama sabini wamechukuliwa,” alisema mmoja wa mkuu wa shule msaidizi wa shule mojawapo ambaye alikataa kutaja jina lake.

Kama ilivyokuwa kwa mwalimu huyo, mmoja wa wenyeviti wa kata hizo naye alikataa kutaja jina, lakini alieleza kuwa kumekuwapo na wanafunzi wanaopelekwa katika shule hizo wakiwa wamepata alama za chini sana katika mitihani ya kumaliza darasa la sababu.

Umbali watajwa
Suala la umbali pia lilitajwa kama sehemu ya changamoto zilizosababisha matokeo hayo mabaya kwa wanafunzi wa shule hizo za Dar es Salaam. Katika Sekondari ya Kitonga, walimu walikutwa wakiwa kwenye kikao na viongozi wa kata kujadili changamoto zilizofanya shule hiyo kushika nafasi ya mwisho.

Akizungumza baada ya kumaliza kikao, Mratibu wa Elimu katika Kata ya Msongola, Venance Mwakilembe alisema bado anafanya utafiti katika shule za kata hiyo zilizofanya vibaya kufahamu sababu ya kwa nini wamepata alama hizo na akipata majibu atapeleka sehemu husika.

Lakini alidai kwa ujumla changamoto kubwa ni watoto kukaa mbali na shule na hakuna mabweni hivyo kutumia muda mrefu kufika shule na kurudi nyumbani.

“Kutokana na usimamizi mbovu wa wazazi ambao wamekuwa wagumu kushirikiana na walimu haijulikani watoto wanafanya nini njiani, lakini wamekuwa watoro na kuibuka kujisajili kufanya mtihani wa mwisho wa kidato cha nne,” alisema Mwakilembe.

Aliweka wazi kuwa katika kikao cha wazazi cha mwisho kwa watoto 200 waliopo shuleni, walifika wazazi 20 pekee huku kuna wakati wazazi waliwapangia wanafunzi vyumba bila kuwa na uangalizi kwa sababu ya umri wao waliishia katika matendo machafu, jambo ambalo shule ililazimika kupiga marufuku.

Katika shule hiyo yenye ikama nzuri ya walimu 26, wana maabara na masuala mengine ya kitaaluma yakiwa vizuri, lakini changamoto ni ya umbali wanaosafiri watoto. Jirani wa shule hiyo, Hassan Waziri anasema serikali inatakiwa kuhakikisha wanafunzi wanaosoma hapo wawe wanakaa karibu au vinginevyo wajenge mabweni.

Wanafunzi waishia njiani
Katika Shule ya Sekondari ya Ndombole, mmoja wa walimu aliyekataa kutaja jina alisema wanafunzi hadi kufika maeneo hayo ambayo yako karibu na shule ya Kitonga, wanatoka maeneo mbalimbali ya jiji, lakini anaeleza kuwa kuanzia watakaomaliza kidato cha nne mwaka huu walianza kupangiwa wanaoishi karibu na shule.

Inaweka bayana kuwa mwanafunzi hadi kufika shuleni anapanda daladala nne kwa anayetokea Buguruni mpaka Gongo la Mboto, Chanika, Mvuti na mwisho anapanda yanayoenda Mbagala na kushuka shuleni anapolazimika kutembea kilometa tatu au kuchukua bodaboda kwa Sh 1,000.

Anaeleza kuwa umbali huo wa shule umesababisha wanafunzi wengi kuwa watoro na kuishia vichakani huku wengine wa kike wakidanganywa na waendesha bodaboda.

Alisema kutokana na changamoto hiyo, walilazimika kutafuta basi la shule lililokuwa likibeba wanafunzi kutoka Buguruni mpaka shuleni na kulipa Sh 2,000 kwa siku, lakini baadhi ya wazazi walikuwa wagumu kulipa kwa kusema ni nyingi hivyo kuacha huduma hiyo.

Alieleza kuwa wanafunzi waliofaulu kwa alama 240 hadi 245 darasa la saba ndiyo wamepata daraja la tatu huku wengine wakifeli kutokana na kuvutwa na waliofeli ambao ni wengi; kama ilivyokuwa kwa shule nyingine zilizovurunda kwa kuchukua wenye alama za chini sana.

Mmoja wa watendaji wa kata hiyo ambaye hakutaka jina lake kuandikwa kwa madai ya kuwa siyo msemaji wa shule hizo, aliweka bayana kuwa alitembelea moja ya shule na kubaini kuwepo mwanafunzi wa kidato cha tatu asiyeweza kuandika kwa ufasaha sentensi ya Kiswahili.

Alisema changamoto ya umbali na kupelekewa wanafunzi waliofanya vibaya mtihani wa darasa la saba nayo ni changamoto kwani wapo waliofaulu mtihani huo kwa wastani mzuri wamepata daraja la tatu.

Katika Sekondari ya Kidete iliyopo kilometa 10 kutoka daraja la Mwalimu Julius Nyerere katika Wilaya ya Kigamboni, inaeleza kuwa ufaulu mdogo wa wanafunzi wanaojiunga kidato cha kwanza shuleni hapo na umbali wa shule kwa wanafunzi ni changamoto shuleni hapo.

Mwalimu wa shule hiyo aliyekataa kutaja jina, alisema kutokana na umbali wanafunzi wengi hufika kwa kuchelewa muda wa masomo kwani wengi wanatokea Yombo Buza na maeneo mengine ya wilaya ya Temeke kwani wanatoka nyumbani saa 10 au 11 alfajiri na kuondoka shuleni saa 8:30 mchana.

Mzazi, mwanafunzi wasifu walimu Katika Sekondari ya Nyeburu, mwanafunzi wa kidato cha pili, Roneco Nziku alisema walimu wanao na wamekuwa wakifundisha vizuri isipokuwa tatizo lipo kwa wanafunzi.

Alisema licha ya kuwa matokeo hayo yanakatisha tamaa, lakini anaamini akijitahidi kusoma kwa bidii hasa masomo ya sayansi anayoyapenda atafanya vizuri kwani shule hiyo ina maabara tatu za masomo ya Kemia, Baolojia na Fizikia isipokuwa tatizo lipo kwa wanafunzi kutozingatia kile wanachofundishwa.

Nziku alisema umbali wa shule kwa wanafunzi ni changamoto kwani wanafunzi wengi hutoka Buguruni na maeneo mengine ya mbali.

Mwananchi anayeishi jirani na shule hiyo, Severino Wami alisema wanafunzi wenyewe wanaonekana hawana nidhamu, lakini pia hawaonekani kama ni watu wanaopenda kusoma kwani huwa hawafiki shule wanakwenda kukaa kwenye mabanda ya mtaani.

“Tunasikia kuna banda moja lipo mtaani ambapo wanafunzi baadhi huishia huko, kitu kingine tunasikia wengi wanatoka maeneo ya mbali kama Buguruni, atatoka saa ngapi arudi ajisomee na kesho awahi, mazingira magumu,” alisema Wami.

Pia alisema hata wazazi wanaweza wakawa ni sababu ya wanafunzi kufeli kwa sababu hawana muda wa kufuatilia viwango au maendeleo ya watoto wao darasani au kama anasoma anaporudi nyumbani.

Naye mzazi wa mtoto Michael Kitumbo anayesoma kidato cha tatu kwenye shule hiyo, Subira Kitumbo, alisema haoni kama walimu wana matatizo kwenye shule hiyo kwani siku zote wamekuwa wakisisitiza umuhimu wa wazazi kushirikiana nao katika kuhakikisha mtoto anafanya vizuri.

Viashiria vilionekana mapema Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Ofisa Elimu wa Mkoa, Janeth Nsunza alisema wakuu wa shule hizo zilizofanya vibaya wametakiwa kujieleza na walianza kutoa maelezo, ikiwa ni sehemu ya hatua walizoanza kuzichukua.

“Mkoa umepokea matokeo hayo kwa masikitiko kwani umekuwa ni kinyume cha matarajio yetu na serikali kwa ujumla kwa kuwa serikali imekuwa ikisisitiza utoaji wa elimu msingi bora kwa wote,” alisema Nsunza.

Alisema viashiria vya matokeo mabaya kwa shule hizo yalianza kuonekana katika matokeo ya mtihani wa majaribio (Mock), jambo ambalo liliwafanya wakurugenzi kuwaandikia barua wakuu wa shule hizo kuongeza juhudi katika masomo ili kuepuka matokeo mabaya katika mtihani wa mwisho.

“Wakati wa mtihani wa Mock, shule hizi zilionesha viashiria vya matokeo mabaya na wakurugenzi waliwaandikia barua wakuu wa shule na kuwataka kuhakikisha wanafanya jitihada ili kuhakikisha shule zao zinakuwa na matokeo mazuri. Lakini tumeona bado hali imekuwa tofauti hawa wanatoa maelezo na mkoa utatangaza hatua za kuchukua baada ya kukamilisha,” aliongeza ofisa huyo.

Nsunza alisema wanafunzi waliofeli ni 619 ambao ni sawa na asilimia 1.1 kati ya wananfunzi 55,980 waliosajiliwa kufanya mtihani mwaka 2016. Aliongeza kuwa shule hizo sita zilizoshika nafasi ya mwisho ni miongoni mwa shule 128 zilizojengwa kwa nguvu za wananchi katika manispaa za jiji hilo.

Wizara yatoa neno
Akizungumzia kufanya vibaya kwa shule hizo, Kaimu Kamishna wa Elimu kutoka Wizara ya Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Nicolas Buretta alisema ipo haja ya kukaa pamoja na mamlaka za Mkoa wa Dar es Salaam ili kufanya uchambuzi wenye kutafuta sababu.

Buretta alisema suala hilo linahitaji utulivu, sio la kuzipata sababu za kufeli kwa shule hizo kwa haraka, bali inahitajika kuwatafuta wadau mbalimbali wa elimu ili kuchambua na kupata kiini cha suala hilo.

“Suala la kuanguka kwa shule hizo sio la kulipatia jibu kwa haraka, ni jambo linalotaka utulivu ili kuweza kuwashirikisha wadau wote na kutafuta sababu za kufeli kwa shule hizo,” alifafanua Kaimu Kamishna wa Elimu.

Kibaha yaibeba serikali Kwa upande mwingine, shule kongwe ya Kibaha mkoani Pwani ni miongoni mwa shule 20 bora, ambayo imeshika nafasi ya 16 kati ya shule 3,280 za sekondari nchini.

Kwa mujibu wa takwimu za viwango vya ufaulu zilizowekwa kwenye tovuti ya Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Kibaha iliyoko Mkoa wa Pwani wanafunzi wamepata daraja la kwanza hadi la nne, na hakuna mwanafunzi aliyefeli.

Kibaha imepanda kwani mwaka 2015 ilishika nafasi ya 69 na mwaka 2014 ilikuwa ya 87. Wakati Kibaha ikiwa ya kwanza kwa ufaulu bora kwa shule za serikali, imefuatiwa na shule ya wanafunzi wenye vipaji ya Mzumbe ya Morogoro iliyoshika nafasi ya 27, na haina mwanafunzi aliyefeli.

Mwaka 2015, Mzumbe ilikuwa nafasi ya 71 na mwaka 2014 ilikuwa ya 56. Shule ya wasichana ya Kilakala imeshika nafasi ya 28 na hakuna mwanafunzi aliyefeli. Mwaka 2015 ilishika nafasi ya 94 na mwaka 2014 ilikuwa ya 96.

Tabora Boys ikishika nafasi ya 41 na kufuatiwa na Ilboru ya Arusha iliyo nafasi ya 42. Shule zingine na nafasi zao kwenye mabano ni shule ya wasichana Tabora (114), Msalato (129), Songea Boys (201), Bwiru (214) na Moshi Sekondari (226).

Kwa upande ya 20 za mwisho, bado inaonekana shule za serikali ndizo zilizoko kwenye eneo hilo kwa kuwa na wastani hafifu. Shule zingine 10 zinazofuatiwa zile zilizotangazwa na Necta ni Mtombozi (Morogoro), Mkikira (Mara), Ndangalimbo na Mnero (Lindi), Ngiresi (Arusha), Piki (Kaskazini Pemba), Kazamoyo (Pwani), Zingiziwa na Sangara (Dar es Salaam), Mugango (Mara) na Mkera (Dar es Salaam).

Imeandikwa na Theopista Nsanzugwanko, Sophia Mwambe, Lucy Lyatuu na Anastazia Anyimike.

No comments:

Post a Comment